Mafundisho ya shule kwa mpangilio wa Kiislamu

“Uislamu ni tajiri sana kwenye upande wa elimu na hakuna elimu ambayo imeiacha. Hivi karibuni tutatoa mwelekeo wa uislamu kwenye elimu, na tutanukuu maneno ya Imaam Ghazali kwenye Ihyaa Uloomud-Diin. Tutatunukuu hapa sehemu ndogo kwa kifupi sana, Imaam Ghazali anasema elimu imegawika kuwa lazima kwa kila mmoja, na elimu iliyokuwa lazima kwa kikundi cha watu, elimu iliyokuwa makruuh na elimu iliyokuwa mubaah na elimu iliyokuwa haramu.

Katika elimu iliyokuwa lazima, kasema si lazima mtu ajue milango yote ya sheria bali ajue kila kinachotakiwa katika muda na hali alionao, akasema kwa mfano si lazima kujua hukumu za Hijja kama hana uwezo na wakati wa Hijja haujafika. Kisha akaendelea kueleza na akasema watu wanahangaika kusoma maelezo ya undani wa sheria na mifano ya mas-ala ambayo hayatokei ila kwa nadra na wakati mjini kwao hakuna daktari wa kike Muislamu wa kutibu wanawake wa kiislamu, na ni jambo la lazima kwa wakazi wa mji na kama halijafanyika wanapata madhambi wakazi wote.

Kwa hiyo ni wazi kuwa baadhi ya elimu tunazoziita za dunia ni lazima tujifunze kwa amri ya dini yetu, na tusipofanya hivyo tutaingia kwenye madhambi makubwa. Maelezo zaidi tutayatoa kwenye makala zetu zijazo.

Wajerumani walivyokuja Tanganyika, wakaona wasomi zaidi ni Waislamu, wanajua kusoma na kuandika, wanajua hesabu na wanatumia tarakimu za kiarabu kwenye maandiko yao, hata lugha ya Kiswahili ilikuwa wanatumia maandishi ya kiarabu. Wakawaajiri hawa kwenye mahakama, na nafasi za Serikali.

Mwingereza alikuja na makusudio yake, ya kuuvunja uislamu na kuwadhoofisha Waislamu, akajenga mashule na kuweka masharti anayetaka kujiunga lazima awe mkristo, ili ajiunge, ndiyo wakati tuliopata majina ya Augostino Saidi na mengineyo. Waliopenda dini yao, wakachukia masomo ya kizungu na kukataa kupeleka watoto wao mashuleni, ili wasiwe wakristo, wakahifadhi dini yao, lakini ikajijenga tabia ya kuchukia elimu za kizungu.

Kwa hakika elimu hizi si za kizungu, ni za Waislamu wenyewe na zinarudi kwao wenyewe, Waislamu waliendeleza elimu na teknolojia, na wafalme wa kiislamu waliwapa zawadi kubwa kubwa wasomi waliovumbua mashine mpya, na zawadi ya kanisa ilikuwa ni kuwaua wanasayansi. Hapo ndipo wakazi wa nchi za kizungu wakaamua kuweka mbali dini na sayansi & Teknolojia. Kitu hicho hakipo kwenye Uislamu. Ndiyo elimu ya secular ilipoanza.

Tukirudi kwenye Tanganyika, nafasi za Serikali zikaanza kuchukuliwa na wakristo, na wakaendelea kupata nafasi hizo, hadi Waislamu walivyoanzisha TANU, hawakuwa na Muislamu wa kushika nafasi ya juu kabisa na kumweka mkristo kwenye nafasi hiyo, na hatimaye wakristo wakaendelea kutawala.

Hiyo ni historia, tusiisahau, lakini pia isiwe ni sababu ya kutupia lawama zote kwa historia, sisi tumefanya nini kuibadili historia hiyo? Waislamu bado kwa asilimia kubwa sana wanachukia elimu za kizungu, na wana hiari wawasomeshe madrasa tu, wasipate elimu za kizungu, au wawasomeshe elimu za kizungu na wasipate elimu za dini, kama wanavyotoka Waislamu wengi hata kwenye shule tunazoziita za Kiislamu. Hakuna sehemu ambapo tumeziweka hizi elimu za kizungu ambazo kwa hakika si za kizungu ziendane na mafunzo ya Uislamu, na kama zipo shule hizo labda hatuzijui.

Kwa kweli njia hizi mbili tumeziweka mbali sana, na hatujajenga njia ya kuzikutanisha, Wanasayansi wakubwa wa kiislamu, wanaanza vitabu vyao kwa Bismillahi, kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumswalia Mtume - Rehema na Amani zimshukie - na bado wanabaki kuwa wanasayansi na wavumbuzi na wazungu wanaiba uvumbuzi wao na kusema wamevumbua wao, bali kushika kwao dini kunawafanya wawe wanasayansi wakubwa zaidi.

Nini cha kufanya ili tusomeshe na tusome hizi elimu za ki-secular, kwa mpango wa kiislamu ???

  1. Walimu Waislamu wa mashuleni wajitolee kuandika masomo ya shuleni bila kubadilisha syllabus kwa mpango wa kiislamu. Kila Sura "chapter" iwe na utangulizi wa aya za Qur-ani na Hadithi kuhusu Sura hiyo, na ndani ya Sura hiyo pia, kuweko na aya ya Qur-ani na Hadithi. Sura hizo pia zitoe mchango wa Waislamu kwenye somo hilo, bali kwenye kipengele hicho pia.
  2. Kuwe na masomo ya dini kwa uhakika wa masomo hayo. Masomo hayo ni kama sheria ya Kiislamu, Sira, Tabia na mambo ambayo yanamuathiri Muislamu kila siku. Isiwe kama shule zetu, tunamfundisha mtoto wetu jinsi ya kutoa hoja za dini, jinsi ya kujibizana na kafiri na asiye na dini lakini ukimwuliza jinsi ya kuswali, hajui, akienda chooni anajisafisha vipi, hajui. Wakati haya ndio masuala muhimu zaidi kuliko kujua kutoa hoja.
  3. Walimu waambizane wenyewe kwa wenyewe umuhimu wa suala hili, walitangaze na kuliendeleza suala hili, na kila mmoja afanye kilicho kwenye uwezo wake. Kila mtu afikishe ujumbe kwa mwenziwe, mwenye elimu atoe mchango wa elimu, mwenye pesa atoe mchango wa kuchapisha vitabu, mashule na kadhalika.
  4. Ikiwa tutasubiri mpaka tuunde Chama, Kamati, Jumuiya ambayo itashughulikia suala hili, hatutafika popote. Tunajua udhaifu wetu, kila mmoja atakuja na makusudio yake, wengine watakuja ili wajaze mifuko yao na matumbo yao, wengine watakuja ili wapate umaarufu, na wengine watawekwa na vikundi ambavyo si vya Waislamu ili waharibu hiyo Jumuiya na mwisho tutavunja Jumuiya yetu. Bora kila mwenye uwezo afanye kilicho kwenye uwezo wake, na anayetaka mwongozo wa jinsi ya kuandika vitabu vya mashuleni kwa mpangilio tuliotaja anaweza kutuandikia (webmaster@uislamu.org) na Insha Allah tutamsaidia kiasi cha uwezo wetu. Pia ambaye anataka kitabu chake kipitiwe, kisahihishwe, au hana uwezo wa kuchapisha pia anaweza kutuandikia.

    Mwenyezi Mungu atupe uwezo wote, wa kuutumikia Uislamu na Waislamu kwa njia bora na ambayo anairidhia Yeye - Aamin.”

MWANDISHI: Makala hii imetolewa ikiwa ni sehemu ya maoni na imekusudiwa kuwa ni changamoto kwa umma, waalimu na wanafunzi wa Kiislamu. Imeandaliwa na Webmaster, www.uislamu.org. Mwenyezi Mungu amzidishie ya kheri juu ya kheri.
TAREHE: Jumamosi, 19 Aprili 2003.

Chagua miongoni mwa machaguo yafuatayo ili kuona kwa kina muhtasari kwa darasa husika

Darasa la Kwanza Darasa la Pili Darasa la Tatu Darasa la Nne Darasa la Tano Darasa la Sita Darasa la Saba

Muhtasari huu umetayarishwa na Islamic Propagation Centre, S. L. P. 55105, Dar es salaam, Tanzania